Saturday, February 2, 2013

NAMPENDA SANA MAMA YANGU

Thuwein Thabit,

Namshkuru sana Mungu muumba wa kila kitu kwa kunijaalia kuwepo duniani kupitia kwenye mgongo wa mama yangu. Shukrani pia ziende kwa mama yangu ambae amesimamia makuza yangu tangu udogoni mpaka ukubwani, na kwa kweli kabisa naweza sema mama ni muhimu katika kila nifanyalo.

Fatma Haji Choum ni mama yangu wa damu ambae amenizaa ambapo kwa bahati nzuri mpaka leo yu hai huku nikimuomba Mungu ampe umri mrefu wenye kheri naye. Nimezaliwa tarehe 29, Ogasti, 1991 katika hospitali ya Mwembeladu. Wakati huo mama yangu alikuwa akiishi mtaa mmoja hapa Zanzibar ujulikanwao kama Migombani. Makero mengi sana nimeyafanya kwa mama yangu wakati nilipokuwa mdogo kama ada ya mtoto kwa mama au mlezi wake. Lakini licha ya yote hayo mama yangu alinipa upendo wa dhati na kunienzi kwa vile nilikuwa ni mtoto wa mwanzo wa kiume katika familia yetu.

Bila ya kusahau mama yangu amechangia mafanikio mengi tu mpaka sasa ambayo nimeyapata. Miongoni mwao ni kuwa nimepata elimu bora na kazi nzuri pamoja na maadili mema ayapasayo kuwa nayo mtoto katika jamii yetu ya Watanzania. Kufuatia yote hayo najihisi ni mwenye bahati sana katika maisha.

Monday, September 17, 2012

Matibabu ya Nairat

IMG_4644



ASALAMU ALAYKUM.
WAKATI tunaendelea kukusanya michango ya watoto wetu Nairat na Bisambe ambao wanasumbuliwa na matatizo ya ngozi, Napenda kutoa taarifa kwamba ahadi ya kwenda hospitali Nairat kulazwa ilikuwa ni tarehe 4 na kufanyiwa upasuaji ni tarehe 5 mwezi ujao inshallah lakini bahati nzuri kumetokea shirika la Kimataifa la Sight savers chini ya mradi wake wa huduma za macho Zanzibar litamdhamini matibabu ya macho Nairat na hivyo kwa sasa badala ya kusubiri mwezi ujayo matibabu yake yatafanyiwa mwezi huu inshallah, ambapo leo hii Nairat na Bisambe wanakwenda Dar es Salaam kwa ajili ya uchunguzi wa macho na hivyo huenda wakalazwa katika hospitali ya Muhimbili badala ya CCBRT na hilo ni kutokana na makubaliano kati ya madaktari wa CCBRT na Muhimbili.

Lakini kwanza kwa kuwa Sight saves wanahusika na macho peke yake tena kwa watoto hivyo basi Nairat ndio atakayenufaika na huduma hii ambayo baada ya kufanyiwa vipimo na kukamilika taratibu zote basi atalazwa hapo Muhimbili na kuendelea na hatua zinazofuata za matibabu. Tumuombee dua inshallah afanikiwe na kila kitu kiwe chepesi kwa uwezo wake Jalali Mola wa uulimwengu wote.
Na baada ya hapo tukishajua suala la macho sasa tutaendelea katika suala la ngozi na katika hilo watalazimika kufanyiwa vipimo wote wawili na tukishajua kitachoendelea tunaendelea kuarifiana lakini kwa sasa tunamshughulikia Nairat ambaye yeye anahitajika matibabu ya haraka kuhusiana na macho yake ambayo yameathirika na kuonekana kuwa ana kensa. Mwenyeenzi Mungu ndio Mjuzi na ndiye mweye uwezo wa kulifanya gumu kuwa jepesi hivyo dua kwa watoto hawa ni muhimu sana kwetu inshallah.
Hadi tulipofikia hapa katika kushughulikia masuala la watoto hawa tunakwenda vizuri Alhamdulillah na mambo yote takriban yanakwenda kwa utaratibu mzuri na kwa wepesi kabisa tunamuomba Mwenyeenzi Mungu atupe nguvu ya kuendelea kushugulikia suala hili hadi kufikia kikomo.

Kwa ufupi kabisa katika suala la hali ya Bisambe ambaye yeye ni mdomo wake ndio wenye kuwa na vidonda na kukatikakatika bado tatizo lake anaendelea nalo licha ya kuchukuliwa vipimo na kutumia dawa kadhaa lakini hajapata unafuu sana ila angalau kidogo hali yake sio kama awali kwa kuwa angalau anaweza kula vizuri kwa sasa ingawa sio nyakati zote hutegemea na yale maumivu anayopata.
Kwa upande wa Nairat vidonda ndani ya macho vimepona, vidonda kwenye pua ndani na nje pia vimekauka ila vidonda katika mdomo bado vinamsumbua ingawa kwa kiasi kikubwa vinaonekana kukauka na kujirudia tena lakini ile kutoka damu tokea nilipomchukua nyumbani kwangu wili ya pili sasa sijaona hata siku moja kutoka damu na ulimi wake sasa naona upo safi vidonda vimekauka na angalau anakula vizuri, na ule mwili wake tokea kuanza kumpaka dawa na kutomruhusu kutoka nje amebadilika na sasa baada ya kufuata masharti ya kutokaa juani ameanza kubadilika rangi ule weusi yaani madodoa meusi katika mwili wake yameanza kufifia na nadhani akiendelea zaidi inshallah yatakwisha ingawa itachelewa lakini naamini atabadilika kwa uwezo wake Allah.

Kuhusiana na fedha tulizopokea hadi sasa tumeanza kuzitumia kwa vipimo mbali mbali tokea walipoanza vipimo vya hapa hapa nyumbani Al Rahma, Mnazi Mmoja na hatimae huko CCBRT na leo huko Muhimbili na pia tumenunua dawa na vifaa ambavyo Nairat ametakiwa kuwa navyo kwa ajili ya kujikinga na jua pamoja na dawa maalumu ambazo anatakiwa atumie muda wote na hivyo risiti zote zipo yaani nakusuadia kwamba hakuna fedha ambayo inatumika au itatumika bila ya maelezo na wala hakuna fedha iliyotoka bila ya utaratibu wa matibabu. Mama Nairat yaani Bi Khadija Mohammed amekubali kutochukua fedha kwa kuogopea kuja kuzitumia kwa shughuli nyengine nje ya lengo yaani ‘matibabu ya watoto’ na hivyo ameniachia mimi kwa ridhaa yake niwe nashughulikia masuala yote hayo. Nami kwa kuwa ameniamini naahidi kwenu nyote mliotoea fedha zenu kwamba fedha hizo zitatumika kwa malengo yaliokusudiwa na inshallah maana lazima tuweke msisitizo wa kumtangulia ALLAH mbele katika suala la fedha kwamba nitajitahidi malengo tuliokusudiwa yafikiwe.
Kwa niaba yangu binafsi na mama mzazi wa Nairat Bi Khadija Mohammed tunawashukuru wote wale ambao wamekuwa karibu sana nasi katika jambo hili kwa kutoa michango yao mbali mbali, kifedha, usafiri, huduma na hata mawazo na kutupa fikra za kufanya katika kufikia lengo la tiba tokea tulipoanza mbio za kutafuta ufumbuzi wa matatizo ya watoto hawa.

Kwa kila hatua tutaelezana inshaalla
IMG_4624 
IMG_4625 
 IMG_4645



Wednesday, September 5, 2012

FAHARI YA WANAUME WENGI MJINI

Hivi nikimzungumzia mwanamke na thamani aliyonayo mbele ya mwanaume sidhani kama nitakuwa nimefanya makosa. Kwa maana ya haraka, mwanamke ni sawa na tunda lenye thamani sana mbele ya mwanamme. Mvuto na ucheshi wa mwanamke huwavuta wengi miongoni mwa wanaume.

Watu wengi hudhani kuwa mwanamke ni chombo cha starehe katika jamii. Usemi huo ingawa hauna uhalisia lakini mara nyengine hudhihirika kuwa ni wenye ukweli ndani yake. Ni jambo la kujivunia sana kuwa kwa namna japo chache sana, Tanzania ni nchi ambayo bado imeendelea kudumisha mila na silka za Mwafrika. Mitaani wasichana wengi hushangaza sana mbele ya wanaume shababi, ingawa huwa ni wabishi. Si jambo la kukanusha kuwa Tanzania katika majia ya miji wanaume hupishana na wanawake ambao huvaa mavazi ya aina kwa aina.

Wanaume wengi huwa ni wenye kuvutiwa na wanawake wanaovaa mavazi yasiyo ya kawaida, na hali hiyo huchochea kuongezeka kwa vitendo vya kujamiiana nchini, hali ambayo huababisha ongezeko la maradhi mbali mbali ya zinaa hasa Ukimwi. Umefika wakati Watanzania wote tubadilikeni!

Thuwein Thabit
05, Septemba 2012